Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Kampasi ya Mizengo Pinda, Dkt. Zacharia Malley, ameongoza shughuli ya upandaji miti katika kampasi kama ishara ya kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuhifadhi mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Dkt. Zacharia Malley, Mwenyekiti wa Bodi, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Kampasi ya Mizengo Pinda akipanda mti
Zoezi hilo limefanyika chini ya kauli mbiu ya kitaifa “Mti Wangu, Taifa Langu,” kampeni iliyoanzishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, yenye lengo la kurejesha uasili wa mazingira, kuongeza uoto wa asili na kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Dkt. Zacharia Malley amesisitiza kuwa upandaji miti ni uwekezaji wa muda mrefu kwa vizazi vijavyo, akibainisha kuwa vyuo vya elimu ya juu vina wajibu wa kuongoza kwa vitendo katika juhudi za uhifadhi wa mazingira, akisema SUA itaendelea kushiriki kikamilifu katika miradi inayolenga kulinda mazingira na kuhimiza jamii kuiga mfano huo.

Dkt. Zacharia Malley, Mwenyekiti wa Bodi, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Kampasi ya Mizengo Pinda akizungumza na wanafunzi na watumizshi wakati wa zoezi la upandaji miti
Kwa upande wake, Rasi wa Ndaki katika Kampasi ya Mizengo Pinda, Prof. Anna Sikira, amesema kampasi hiyo imejipanga kuhakikisha miti yote inayopandwa inatunzwa na kusimamiwa ipasavyo hadi ikue, kwa lengo la kutengeneza mazingira rafiki kwa shughuli za kimasomo, utafiti na ustawi wa jumuiya ya chuo kwa ujumla.

Prof. Anna Sikira, Rasi wa Ndaki katika Kampasi ya Mizengo Pinda, akishiriki zoezi la upandaji miti








