Mkuu wa Wilaya ya Kaliua, Mheshimiwa Gerald Mongera, amekipongeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Kampasi ya Mizengo Pinda, kwa kuwa mstari wa mbele katika kuleta mapinduzi ya kiteknolojia kwenye sekta ya ufugaji nyuki nchini kupitia mafunzo ya vitendo na bidhaa bora.
Pongezi hizo amezitoa leo alipotembelea banda la kampasi hiyo katika Maadhimisho ya Wiki ya Nyuki Kitaifa yanayofanyika Mkoani Tabora kwenye Viwanja vya Kumbukumbu ya Vita.
Akiwa bandani hapo, Mheshimiwa Mongera alipokelewa na kupatiwa maelezo ya kina kutoka kwa Carine John Singu, mwanafunzi wa mwaka wa pili anayesoma Shahada ya Awali ya Usimamizi wa Rasilimalinyuki (Bachelor of Science in Bee Resources Management).

Mwanafunzi huyo alimweleza Mkuu wa Wilaya kuhusu kozi za kimkakati zinazotolewa chuoni hapo, pamoja na kuonyesha vifaa vya kisasa vinavyotumika katika kujifunzia, uvunaji, na uchakataji wa asali safi na mazao mengine ya nyuki.
Mh. Mongera alivutiwa na namna chuo kinavyochanganya nadharia na vitendo, hasa kwa kuona mizinga ya kisasa na vifaa vya uchakataji vinavyoandaliwa na wataalamu pamoja na wanafunzi wenyewe kupitia karakana na viwanda vya chuo.

“Hivi ndivyo vyuo vyetu vinatakiwa kufanya. Sio tu kutoa vyeti, bali kutoa wataalamu wenye ujuzi wa vitendo na uwezo wa kubuni vifaa vinavyoenda kutatua changamoto za wafuga nyuki wetu kule vijijini na kuongeza thamani ya asali yetu,” alisema Mh. Mongera.

Kwa upande wake, Carine alibainisha kuwa elimu wanayopata SUA Kampasi ya Mizengo Pinda inalenga kumjenga mwanafunzi kuwa mjasiriamali na mshauri wa masuala ya nyuki, ili akihitimu aweze kujiajiri na kuajiri wengine badala ya kusubiri ajira za serikalini.

Maadhimisho ya Wiki ya Nyuki Kitaifa yanaendelea mkoani Tabora, huku banda la SUA Kampasi ya Mizengo Pinda likiwa kivutio kikubwa kwa wananchi, wadau wa mazingira, na viongozi mbalimbali wanaotaka kujifunza mbinu za kisasa za ufugaji nyuki wa kibiashara.




